MAWAZIRI watatu wa Rais Jakaya Kikwete juzi walizomewa baada ya
kupanda jukwaani kujibu kero mbalimbali za wananchi katika mkutano wa
kwanza wa viongozi wapya wa CCM taifa, ulioongozwa na Katibu Mkuu wake,
Abdulrahaman Kinana.

Tukio hilo lilitokea juzi mkoani Mtwara ambako
Kinana na mawaziri hao walikuwa katika ziara ya chama kujibu kero
mbalimbali za wananchi.Mawaziri waliokumbwa na dhahama hiyo ni
Christopher Chiza wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Hawa Ghasia (Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa - Tamisemi) Naibu wake, Aggrey Mwanri.
Chiza
ndio alikuwa wa kwanza kukumbana na zomeazomea hiyo, lakini mambo
yalikuwa magumu zaidi kwa Ghasia ambaye alizomewa tangu alipoanza
kuzungumza mpaka alipomaliza.Ghasia ambaye pia ni mbunge wa Mtwara
Vijijini, alirushiwa makombora na Rukia Ismail Athumani ambaye
alimshutumu yeye pamoja na Mbunge wa Mtwara mjini, Asnein Murji kwamba
waliruhusu gesi kupelekwa Dar es Salaam wakati wananchi wa mkoa huo
hawajafaidika nayo.
“Ghasia na Murji kwanini mnaudanganya umma
kwa kupeleka gesi Dar es Salaam, sisi hatuna ubaya na chama ila hatutaki
gesi iende huko” alisema Athumani huku akishangiliwa na mamia ya watu
waliohudhuria mkutano huo.Kabla ya dada huyo kuteka hisia za wananchi
kwa kuwasilisha kero hiyo, Kinana alimruhusu mwananchi mwingine, Issa
Kambona ambaye pia alieleza kuwa hakubaliani na suala la gesi hiyo
kupelekwa Dar es Salaam.
Kinana alisema amesikia hoja hizo za
wananchi na kwamba atamueleza Waziri wa Nishati na Madini azungumze na
wananchi wa Mtwara kuhusu gesi hiyo.Baada ya mambo kuzidi kuwa magumu,
Ghasia alilazimika kupanda jukwaani kujibu makombora aliyokuwa
akirushiwa na wananchi waliofika katika mkutano huo.
“Sio kweli
kwamba hatutetei maslahi yenu, gesi iliyopo ni nyingi hamuwezi kuitumia
na kuimaliza, kuna futi za ujazo trilioni 20,000 na tunaweza kuitumia
kwa zaidi ya miaka 90, hata hivyo, Wizara ya Nishati na Madini imetoa
ofa ya kuwalipia chuo vijana 150 kila mwaka,” alisema Ghasia, lakini
wananchi hao waliendelea kumzomea.“Uongo, uongo, hatutaki, hatutaki,
huyoo, huyooo” walisikika wakisema wananchi hao, hali iliyomfanya Katibu
wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye kuingilia kati,
kujaribu kuwatuliza.
“Kelele unazozisikia dada (Ghasia)
zinaashiria kuna jambo, nafasi hizo 150 hawazipati, kama zinatolewa basi
kwa upendeleo,” alisema Nape huku akishangiliwa na wananchi hao.Baada
ya hali kutulia kiasi, Ghasia alijaribu kuendelea kutoa ufafanuzi,
lakini kitendo cha kuanza kuzungumza, wananchi hao walianza tena
kuzomea.
“Kila mtu amelelewa katika mazingira tofauti, hilo
halinihusu…watu wangu wa Mtwara vijijini wamenielewa,” alisema Ghasia na
kuteremka jukwaani hali iliyozidisha kelele za kumzomea.Nape
alisawazisha mambo kwa kusema, hoja ya wananchi hao imechukuliwa na
itawasilishwa kwa Serikali ili kuona namna ambavyo inaweza kukaa na
wananchi hao na kuweka maslahi yao mbele.
Ilivyoanza
Panzia la
zomea zomea lilifunguliwa na Chiza alipopanda jukwaani kujibu hoja ya
kuyumba kwa soko la zao la korosho, ambapo wananchi walimpinga baadhi ya
kauli alizozitoa.“Tatizo la korosho ni baadhi ya viongozi wa vyama vya
ushirika na wengine ni watendaji wa Serikali …nipo hapa na wala
siondoki, nitalishughulikia hili ili korosho zinunuliwe” alisema Chiza
huku sauti za wananchi zikimpinga kwa kusema “uongooo”.
Hata
hivyo, Chiza aliweza kukabiliana na hali ya zomeazomea jukwaani baada ya
watuliza wananchi kwa kusisitiza kuwa ataendelea kuwapo Mtwara,
kushughulikia tatizo hilo ili ununuzi uendelee.Naibu Waziri wa Tamisemi,
Mwanri alipata wakati mgumu mara alipopanda jukwaani na kuanza
kuzungumzia namna ya kumaliza kero ndogondogo zinazoletwa na mamlaka
zake, wananchi walikuwa wanazoea “huyoo…hatutaki” lakini baada ya kuanza
kuongea alionekana kuiteka hadhira na mambo yakawa shwari. “
“Tumesema
wauza vitumbua, wasibughudhiwe … mkurugenzi njoo jukwani, nakuagiza
kuanzia leo marufuku wanafunzi kurudishwa shuleni kwa sababu ya
michango” alisema Mwanri huku akishangiliwa.Awali Kinana alisema mkutano
huo unalenga kuzipatia ufumbuzi kero za wananchi ambazo zinawezakuwa
kikwazo kwa chama hicho kuingia madarakani mwaka 2015.
Katibu
mkuu huyo wa chama tawala alisema umefika wakati wa chama kusimamia
utendaji wa Serikali kutatua kero za wananchi wa mkoa wa Mtwara ikiwa ni
pamoja na kuyumba kwa soko la korosho na gesi.“Najua hapa kuna kero
kubwa mbili, korosho na gesi, nimekuja na Mawaziri hapa watatoa majibu
leo” alisema Kinana huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu
ulioudhuria mkutano huo.
Sifa mgombea urais
Katika hatua
nyingine, Kinana amevunja ukimya kuhusu mbio za urais mwaka 2015 na
kusema CCM itamtosa bila kumuonea haya mwanachama yeyote atakayeomba
kuteuuliwa kugombea urais kwa tiketi yake, huku akiwa kinara wa
kutegemea makundi kumwigiza katika nafasi hiyo.Badala yake akaeleza kuwa
chama hicho kitamteua mgombea mwadilifu, anayekubalika na watu na asiye
na makundi.
Mbali na sifa hizo Kinana pia ameeleza kuwa mgombea
huyo wa CCM atakuwa msafi, makini, mchapakazi, mzalendo ambaye anajali
maslahi ya wananchi na kwamba Mei 2015 wataanza kutoa fomu kwa wana CCM
wanaowania nafasi hiyo.Kinana alisema hayo jana katika kijiji cha Isesa,
Sumbawanga Mjini wakati akifungua tawi la CCM na kuzungumza na
wanachama.
Katika kipindi cha kuuliza maswali, wanachama hao
walitaka kufahamu namna chama hicho kilichojipanga kumpata mgombea urais
makini ambaye hatakuwa mzigo kumnadi dhidi ya wapinzani.“Tumejipanga
vizuri, atapatikana mgombea urais bora, vigezo vipo wazi tunataka
mgombea urais mwadilifu, makini, mchapakazi, mzalendo ambaye anakubalika
na wananchi,”alisema Kinana.
Aliongeza kwamba chama hicho
kitatoa fomu kwa wanaotaka kuwania nafasi hiyo na vikao vya chama ndivyo
vitakavyoamua,”alisema Kinana.“Tuna utaratibu mzuri wa kupata wagombea
urais bora kwa sababu vigezo vyote viko wazi na kwamba wagombea hao
watapimwa kwa vigezo hivyo,” alisema Kinana.
Alisema
Wanasumbawanga wasiwe na wasiwasi watampata mgombea ambaye atakuwa mwiba
kwa vyama vya upinzani.Alisema kiongozi mwenye makundi na asiyekuwa
mwadilifu hatakuwa na nafasi ya kuteuliwa na chama hicho kugombea
urais.“Haya si maneno yangu bali ni vigezo vya chama vilivyo wazi
ambavyo vinatumiwa kwa kila mgombea wa nafasi hiyo kubwa kushinda zote,”
alisema
Alisema anakifahamu chama hicho na kwamba kitavitumia
vigezo hivyo ili kupata mgombea urais ambaye wananchi wanamkubali.Awali
wanachama wa chama hicho wakiongea kwa hisia kali, walisema wanataka
chama hicho kimsimamishe mgombea urais atakayekuwa mwiba kwa wapinzani.
“Tunayasikia
majina ya watu wanaowania nafasi hizo, chonde chonde katibu mkuu
tunaomba apatikane kiongozi ambaye hatatupatia kazi ya kumnadi, awe
mwadilifu ambaye akitangazwa watu wafurahi bila kunung’unika,” alisema
Peter Lilata.Alisema, “tukikosea kuteua kiongozi bora tutakuja kujuta
hapo baadaye.”
Vijana CCM, Chadema nusura wazipige
Katika
ufunguzi wa tawi la CCM la Isesa nusura vijana CCM na wa Chadema
watwangane makonde baada ya vijana wa Chadema kuwatuhumu CCM kwamba
wamewaibia bendera ya chama chao.