April 2025

 Barrick Tanzania yenye ubia na serikali kupitia kampuni ya Twiga imenyakua tuzo kumi za kimkakati katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Afya na Usalama Mahali pa Kazi (OSHA) ya 2025 iliyofanyika mjini Singida ambapo Mgodi wa Barrick Bulyanhulu umeshinda tuzo kubwa ya mshindi wa juu wa jumla katika kipengele cha Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) na Mgodi wa North Mara kuwa mshiriki bora wa maonesho ya mwaka huu (Overall Best OHS Exhibitor- North Mara)  

Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Bi Zuhura Yunus akitoa moja ya tuzo kwa wafanyakazi wa kampuni ya Barrick kwenye hafla hiyo 

Tuzo zingine ambazo Migodi ya Barrick Bulyanhulu umeshinda ni Usalama katika Kuchimba maeneo hatarishi (Advancing in High-Risk Mining Operation), Utoaji wa maelezo kwa ufasaha kwenye maonesho (Best Narrator) na Tuzo bora ya Ubunifu (Best OHS Innovator award).

Waziri wa Nchini Ofisi ya Waziri Mkuu , (Ajira, Kazi na watu wenye ulemavu) Ridhiwani Kikwete akikabidhi tuzo kwa Mrakibu wa Usalama Mgodi wa Barrick North Mara , Meshack Issack

Barrick North Mara walishinda tuzo za Ujumuishaji Wafanyakazi wenye mahitaji maalum katika Maonesho (Inclusion of Workers with Special Needs Award), Usalama katika kuchimba maeneo hatarishi (Advancing in High Risk Operation), Mshindi wa Jumla kwenye washiriki (Overall best OHS Exhibitor) na mshindi tatu kwenye Uwajibikaji wa Jamii (CSR)

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Bi Mary Maganga akikabidhi tuzo kwa Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Zonnastraal Mumbi kwenye hafla hiyo 

Kwa upande wake Barrick Buzwagi walikuwa washindi wa tatu kwenye taaluma ya Ufundi wa kisayansi (Professional and Technical Scientific award) na tuzo ya uwezeshaji wa maonesho (Special recognition of Outstanding support) 


Katika Hafla hiyo ambayo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Nchini Ofisi ya Waziri Mkuu (Ajira, Kazi na Watu Wenye Ulemavu) Mhe, Ridhiwani Kikwete ambaye alisisitiza umuhimu wa waajiri na wafanyakazi kuzingati sheria, kanuni na miongozo inayotolewa na serikali kupitia Wakala wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi (OSHA) ili kumlinda mfanyakazi na uwekezaji na biashara kwa ujumla.


Naye Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Afya na Usalama Mahali pa kazi (OSHA), Bi Khadija Mwenda alitumia nafasi hiyo kuwashukuru washiriki wote, waajiri na wafanyakazi kwa kuendelea kuzingatia kanuni na sheria za afya na usalama mahali pa kazi kama injini ya kuongeza uzalishaji kwenye maeneo yao ya kazi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchini kwa ujumla. 



Wafanyakazi wa Barrick wakifurahia ushindi katika hafla hiyo


Mwakilishi wa Barrick katika hafla hiyo ambaye ni Mrakibu wa Usalama , Mgodi wa North Mara Bw. Meshack Issack alisema Barrick -Twiga itaendelea kushirikiana na serikali katika kulinda afya za wafanyakazi wake pamoja na kudumisha usalama kama nyenzo ya kuchochea uzalishaji , ufanisi na matumizi ya akili mnemba katika sekta ya madini hapa nchini.


Ushindi wa mwaka  huu ni mwendelezo wa ushindi katika maonyesho ya OSHA yaliyofanyika katika miaka ya karibuni ambapo mwaka jana pia kampuni ilishinda tuzo tano ikiwemo tuzo ya mshindi wa jumla.


Suala  la Afya na Usalama ni DNA ya kampuni ya Barrick na  imeendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa za kidigitali na akili mnemba kuhakikisha inaimarisha zaidi usalama kwenye maeneo yake ya kazi na inatekeleza program za usalama ya Journey to Zero na kufanikisha kutokomeza matukio ya ajali kazini na nje ya kazi kwa wafanyakazi wake.


Mbali na kuwekeza katika usalama, Barrick imeendelea kuchangia pato la Serikali kupitia kodi na tozo mbalimbali, Kutekeleza miradi mikubwa ya kijamii kupitia fedha za CSR zinazotolewa na migodi yake hususani katika mikoa ya Mara ulipo mgodi wa North Mara na Shinyanga na Geita ulipo mgodi wa Barrick Bulyanhulu hususani katika sekta za afya, elimu na miundombinu ambayo imebadilisha maisha ya Wananchi kuwa bora zaidi.

Pia kampuni imekuwa kinara wa kutekeleza sera ya Maudhui ya ndani (Local content) ambayo inaendelea kuwanufaisha wazawa kwa kufanya kazi na migodi yake.











 Ni Sakata la kiwanja namba 170A kipawa jijini Dar es Salaam  

Sakata hilo la kiwanja limefika kwa Waziri Mkuu 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam 

Mfanyabiashara tajiri mwenye asili ya kiasia, Bw Satesh Khumal anatuhumiwa kukaidi wito Mawaziri wawili kwa nyakati tofauti wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuhusu kupeleka wizarani nyaraka halali za umiliki wa kiwanja namba 170A eneo la kipawa, Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam. 

Mawaziri hao ni Jerry Silaa na Deogratias Ndejembi wa sasa ambao kwa nyakati tofauti walimuita Mfanyabiashara huo kupeleka nyaraka halali za umiliki wa kiwanja hicho ili kuweza kutatua mgogoro wa eneo hilo ambao umedumu kwa takribani miaka 14.

Waziri wa Ardhi, nyumba na Maendeleo ya Makazi, Deogratias Ndejembi

Taarifa ambazo mwandishi wa habari hii amezipata ni kwamba Jerry Silaa na Deogratias Ndejembi walifanya juhudi za makusudi kuweza kusuluhisha mgogoro wa eneo hilo ambalo ni mahususi kwa ajili ya maendeleo ya viwanda (Industrial area).

Taarifa zinasema kwamba eneo hilo lilikuwa miliki ya marehemu wawili, Asha Binti Mwinyikondo na Buna Binti Musa ambao ni ndugu wa kuzaliwa na walikuwa na hati ya mkoloni na walianza kumiliki eneo husika hata kabla ya Uhuru wa Tanganyika 1961. 

Ambapo baadaye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Chini ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ilichukua sehemu ya eneo hilo na Kujenga reli ya Tazara.

Baada ya kufa wamiliki hao wa eneo husika , ndipo  Bi Mwanaidi Alawi akachaguliwa na familia kuwa msimamizi wa mirathi wa eneo hilo la marehemu hao wawili amba oni shangazi zake, ambapo ndugu zake wameithibitishia mwadishi  kwamba Bi Mwanaidi Alawi alifariki dunia mwaka 2016.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii kwenye mahojiano maalumu, Msimamizi wa mirathi ya marehemu Bi Mwanaidi Alawi, Ndugu Mbwana Alawi alisema kwamba mgogoro wa eneo husika ulianza kufukuta rasmi baada ya kifo cha shangazi yake Bi Mwanaidi Alawi ambaye alifariki dunia 2016 na kulazimika kukimbilia wizarani ili kuweza kupata msaada.

“kwa ujumla kampuni hii ya Petro Fuel imekaidi maelekezo ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Deogratias Ndejembi ya kukabidhi kiwanja namba 170A eneo la kipawa , Wilaya ya Ilala kwangu kwa sababu tayari Waziri amenipatia hati namba 149078”

 

Aliongeza kwamba huyu mmiliki wa Petro fuel aliitwa mara kadhaaa toka mwezi wa tano mwaka jana hadi tarehe 3 mwezi machi mwaka jana na kutofika kwake kulitolewa maamuzi ya mimi kupewa hati nyingine na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

“Na hati hiyo nilipewa baada ya kutoka tangazo kwenye gazeti kwa siku 30 zikapita Bila pingamizi lolote na wizara kutoa hati halali kwangu pamoja na Waziri Ndejembi kutoa maelekezo ya kampuni ya Petro Fuel kuondoa walinzi wake kwenye kiwanja husika lakini bado kampuni hii imekaidi maagizo hayo ya Waziri,” alisema kwa masikitiko makubwa

Alifafanua zaidi baada ya maamuzi hayo ya Waziri , Bw Mbwana Alawi akiwa na mjomba wake mwingine walitembelea eneo hilo lakini cha kushangaza walikamatwa na Polisi kutoka kituo cha Buguruni na kuwekwa ndani na kufunguliwa kesi ya kutishia kuua kwa kutumia silaha na mpaka leo kesi hiyo bado ipo kituoni.

Mwandishi wa Habari hii alifanya juhudi za kumtafuta Waziri mwenye dhamana ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi , Bw Deogratias Ndejembi ili kuweza kujua Sakata hili ambapo lilifika mezani kwake alilitolea maamuzi.

Alipotafutwa kwa njia ya simu ya kiganjani kupitia (whattsap) Waziri Ndejembi aliomba atumie maelezo ya mgogoro wa kiwanja ngani na ni eneo lipi na alipotumia na mwandishi akasema apewe muda akirudi ofisini ataangalia mpaka tunakwenda hewani bado hatujapata majawabu ya Waziri kama ni kweli alitoa hati mpya kwa Bw Mbwana Alawi na juhudi zinaendelea kumtafuta.

Msimamizi wa mirathi wa eneo hilo , aliongeza kwamba nyakati tofauti aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa alimtaka mmiliki wa kampuni ya Petro Fuel Bw Satesh Khumal ambaye ni  mfanyabiashara mwenye asili ya kiasia kufika wizarani ili kuleta nyaraka muhimu za umiliki wa kiwanja hicho ambaye mara kadhaa alishindwa kufanya hivyo na kutuma wasaidizi wake ambao waliwasilisha nyaraka na saini zilizoghushiwa.

Kwa Mujibu wa Bw Mbwana Alawi Petro Fuel kupitia msaidizi wa Tajiri huo mwenye asilia ya kiasia Bi Mashamsham Dorice wanadai kwamba  mwaka 2013 walimpa Mwanaidi Alawi kiasi cha Tsh 20 milioni.

“Ni kweli shangazi yangu alichukua fedha taslimu hizo na hata mwaka 2015 walimpa kiasi cha Tsh 30 millioni marehemu shangazi yangu ,Bi  Mwanaidi Alawi na aliweka saini ya dole gumba maana alikuwa hajui kusoma na kuandika,” alifafanua Bw Mbwana. 

“kwenye haya malipo ya awali ni kweli shangazi alipokea ila alisema fedha nyingine inayobaki kiasi cha Tsh 610 milioni kiwekwe kwenye benki  ambapo kampuni hiyo ya Petro Fuel haijafanya hivyo mpaka umauti unamfika,” alisema Mbwana Alawi, Msimamizi wa mirathi.

Bw Alawi alisema kwamba nyaraka walizoleta kampuni ya Petro Fuel wizarani ni kwamba uhamisho wa umiliki wa eneo (Valuation Transfer) malipo yanaonyesha na saini yalifanyika 2018 na 2019 ambapo tayari shangazi yake mwanaidi Alawi alikuwa ameshafariki.

“Jambo la kushangaza ni kwamba nyaraka zao za mwaka 2018 na 2019 ya uhamisho wa umiliki kutoka kwa Mwanaidi Alawi kwenda Petro Fuel ilifanyika wakati shangazi alikuwa ameshafariki na saini yake wakati alikuwa hajui kusoma wala kuandika inashangaza kwa kweli,’ alisema kwa uchungu  

Bw Mbwana Alawi alisema kwamba wakati , Jerry Silaa akiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi , lilifika mezani kwake swala hili na likaanza kushughulikiwa na maafisa wa wizara na Kamishina wa Ardhi wa Mkoa wa Dar es Salaam.

Katika moja ya barua ambayo mwandishi wa habari hizi amezipata kutoka kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ya 24/05/2024 kwenda kwa kampuni ya Petro fuel iliyoitaka kampuni hiyo kuwasilisha nyaraka za umiliki wa kiwanja tajwa iliyosainiwa, barua hiyo ilisainiwa na  Bw Burton Rutta kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam.

“ila cha kushangaza mara kadhaa alikuwa akiitwa na kuandikiwa barua rasmi za serikali ikimtaka aweze kufika kuleta nyaraka za umiliki wa kiwanja , hafiki isipokuwa alifika mara moja na msaidizi wake , Bi Mashamsham Dorice na alileta nyaraka ambazo zinasaini ya Bi Mwanaidi Alawi , wakati shangazi yangu alikuwa hajui kusoma na kuandika na kuweka saini alikuwa anatumia dole gumba,” alisema Bw Mbwana Alawi 

Wakati huo huo , Mwandishi wa Habari hii pia alifanya juhudi za kumtafuta Bi Mashamsham Dorice wa kampuni ya Petro Fuel ili kupata maelezo na ufafanuzi kwa upande wao ili alisema kwamba yupo nje ya ofisi akirudi ataweza kuwa na ufafanuzi.

Pamoja na juhudi za kumpigia simu yake ya kiganjani na kutuma ujumbe wa sms kupitia njia ya whattsap na maswali kadhaa , Bi Dorice alishindwa kutoa ufafanuzi au kujibu sakata la kiwanja hicho mpaka tunakwenda mitamboni.

Taarifa ambazo zimemfikia mwandishi wa habari hii na baadhi ya vyombo vya habari nchini ni kwamba sakata hilo la mgogoro huo wa kiwanja limefika mezani kwa Waziri Mkuu , Kassim Majaliwa na tunaendelea kulifuatilia kwa karibu.

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.