Na Damas Makangale, Makangale Satellite Blog

“Kila mwaka idadi ya watumiaji wa dawa za kulevya nchini hasa kwa vijana wenye umri mdogo kabisa kati ya miaka 15 mpaka 25 inakadiliwa kufika 10,000 hadi 11,000 kila mwaka nchini ni idadi kubwa na hali inatisha,’ anasema Afisa kutoka Kitengo cha Kudhibiti dawa za kulevya nchini, Moza Makumbuli 
 
..Ni baadhi ya watumiaji wa dawa za kulevya wakihudhuria moja semina zinazoendeshwa nchini
Wiki iliyopita Kitengo cha Kudhibiti Dawa za Kulevya Nchini ( Drug Control Commission) kiliandaa semina ya siku moja kwa wadau mbalimbali kutoka kwenye vyombo vya habari, magereza, Polisi, Mashirika yasiyo kuwa ya Kiserikali, Madaktari na wizara ya afya na lengo la semina hiyo ilikuwa kuwapa wadau matokeo ya utafiti ya watumiaji wa dawa za kulevya cocaine na heroin nchini.

Akizungumza na wanasemina hiyo, Bi Makumbuli amesema kwamba utafiti huo ulifanyika katika mikoa 12 ya Tanzania bara kwa kufanya mahojiano na watumiaji, waathirika, wananchi wa kawaida, polisi na watu mbalimbali pamoja na watoa taarifa ikiwemo na utafiti wa mahali husika.

Amesema kwamba utafiti huo ulifanyika katika mikoa ya Mtwara, Dodoma, Morogoro, Pwani, Kilimanjaro, Tanga, Arusha, Mwanza, Mbeya, Shinyanga, Geita na kigoma.

Lengo linguine la utafiti huo wa kisayansi ni kuongeza uelewa wa athari za matumizi ya dawa za kulevya, hatari ya watumiaji kupata maambukizi ya virusi vya ukimwi na tatizo la wagonjwa wa akili nchini inayochangiwa na matumizi ya dawa za kulevya nchini.

Bi Makumbuli aliongeza kwamba matumizi ya dawa ya kulevya kwa njia ya kujidunga kwa sindano imeongezeka maradufu Duniani na Kusini Mwa Jangwa La Sahara ambapo takribani watu milioni 13 wanatumia dawa hizo za kulevya kati ya heroin na cocaine duniani na kusini mwa jangwa la sahara takribani watu milioni 1.5 wapo kwenye matumizi ya dawa hizo.

Alifafanua kwamba tatizo la madawa ya kulevya nchini halikupata nafasi ya kuhifadhi kitakwimu au taarifa zake nyingi hazijapata nafasi ya kuwekwa vizuri kwenye kumbukumbu (Well documented) kwa muda mrefu na ndiyo kikwazo kwa serikali kuamua, kupanga na kuchangua mikakati madhubuti ya kupambana na ongezeko hilo la uuzwaji na utumiaji wa madawa hayo ya kulevya nchini.

“kwenye utafiti wetu tumegundua kwamba sehemu nyingi za pwani (Coast Region) na pembezoni mwa barabara (Along the road corridor) zimeathirika sana kwa vijana wengi kujihusisha na uuzwaji na utumiaji wa madawa hayo ya kulevya na wengi kazi zao ni makodakta wa daladala, wapiga debe, wavuvi sehemu za pwani na wengine ni vibaka na wanawake wanajihusisha na biashara ya ukahaba,” aliongeza.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu ya kudhibiti dawa za kulevya kutoka kitengo hicho cha serikali, Bw Joel Ndayongeje amesema kwamba mapambano dhidi ya dawa za kulevya bado yana safari ndefu hapa Tanzania kutokana na kusongwa na vikwazo lukuki vikiwamo vya sheria dhaifu, ukosefu wa sera ya Taifa ya udhibiti na kuendekezwa kwa vitendo vya rushwa katika vyombo vya dola.

Bw Ndayongeje aliongeza kwamba kwenye utafiti wao waligundua pia mikoa inayoongoza kwa matumizi makubwa ya dawa za kulevya nchini ni 5,190,  Tanga, 3,300 Mwanza, 2,700 Arusha, 1,539 Morogoro, 1,096 Dodoma, 820 Mbeya, 563 Kilimanjaro, 319 Shinyanga, 108 Geita, 100 Kigoma na watu 65 mtwara. 

Amesema kwamba katika miaka ya hivi karibuni matumizi ya dawa za kulevya kwa wanawake yameongezeka mara ya mwisho ulifanyika na kupata matokeo ya asilimia 6% lakini utafiti wa hivi karibuni kwa kushirikiana na Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na magonjwa cha wa marekani (US Centres for Disease and Prevention (CDC) nchini idadi ya wanawake kwenye matumizi ya dawa za kulevya kwa sasa ni asilimia 20%
Pamoja na mambo mengine Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliwahi kukiri kuwa tatizo la dawa za kulevya hapa nchini ni kubwa, linalohitaji nguvu kubwa ya mataifa yote duniani.

“Mapambano dhidi ya dawa za kulevya hayatafanikishwa na nchi moja bali nchi zote duniani,” amesema Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati akiliahirisha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Dodoma, Septemba 6, mwaka jana.
Kutokana na ukubwa wa tatizo hilo, Pinda anasema Serikali inafikiria kuanzisha mahakama maalumu ili kuharakisha mashauri ya dawa za kulevya.

“Nina imani tukijipanga vizuri inawezekana… tutafika mahala tufikirie mahakama maalumu ya dawa za kulevya ambayo itakuwa na kazi moja tu ya kusimamia mashauri yanayohusu dawa za kulevya,” anasema.

Kadhalika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, anasema Serikali inaandaa mapendekezo ya kufuta Sheria ya Dawa za Kulevya na kutungwa mpya itakayokidhi mahitaji ya kushughulikia ipasavyo makosa ya dawa za kulevya.

Wakati Serikali ikitangaza msimamo wake huo, meli iliyosajiliwa Tanzania (upande wa Zanzibar) iliripotiwa kukamatwa nchini Italia ikiwa imesheheni tani 30 za dawa za kulevya zenye thamani ya paundi milioni 50, sawa na Sh bilioni 123 za Tanzania.

Kutokana na mazingira hayo, Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya nchini (DCC) kwa upande wake, inaona pia kuna haja ya Serikali kutangaza dawa za kulevya kuwa adui namba moja kama hatua mojawapo ya kuonesha ukubwa wa tatizo hilo hapa nchini lakini watafanya hivyo endapo tu kutakuwa na ushahidi wa kitafiti na kitakwimu ili kuweza kujenga hoja hiyo.

Heroin na madhara yake
Heroin ni aina ya dawa ya kulevya ya unga inayopumbaza mfumo wa fahamu. Dawa hiyo inatokana na mmea uitwao ‘opium poppy’. Imekuwa ikiingizwa hapa Tanzania ikitokea nchi za Mashariki ya mbali.

Mitaani heroin huitwa majina mengi kama vile unga, brown shugar, ngoma, ubuyu, mondo, ponda, dume, farasi, n.k.
Cocaine na madhara yake
cocaine ni dawa ya kulevya inayotengenezwa kutokana na mmea wa coca ambao hustawi zaidi katika nchi za Amerika ya Kusini. Kitaalamu mmea huo hujulikana kwa jina la erythroxylon coca.

Cocaine, kwa mujibu wa watafiti , huwa katika unga mweupe au katika hali ya mawe madogo madogo. Inajulikana kwa majina mengi kama vile snow, star dust, keki, unga, big c, bazooka, white sugar na unga mweupe.

Hapa Tanzania cocaine hupatikana kwa shida kwa sababu ya bei yake ni nadra sana kupatikana nchini.


Anataja madhara ya cocaine kuwa ni kuathiri mfumo wa fahamu wa binadamu, kutokwa na damu puani, kuwa na mafua makali yasiyopona, kukosa hamu ya chakula, kupanuka kwa mboni za macho, mchafuko wa damu na kupata majipu, kuongezeka kwa mapigo ya moyo na shinikizo la damu.

Madhara mengine ya cocaine ni mtu kuchanganyikiwa, kukosa ufanisi kazini, kuwa na hisia za kuwapo kwa vijidudu mwilini, magonjwa ya ini, kuharibika kwa mishipa ya fahamu, kuharibika kwa moyo, figo na mapafu, kikohozi cha muda mrefu, kupasuka kwa mishipa ya damu kichwani kunakoweza kusababisha kiharusi au kifo na kumweka mtu katika hatari ya kuambukizwa virusi vya Ukimwi.
 
Mtumiaji wa kujinduga akitumia dawa hizo
Mwisho.







Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.