MUUNGANO wa makampuni kadhaa kutoka nchini Oman, umetangaza uwekezaji wa kihistoria kwa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).

Muungano huo, umekusudia kutoa Sh bilioni 160 kwa ajili ya mambo mbalimbali, yakiwamo ya kununua ndege mpya na za kisasa na ujenzi wa kituo cha mafunzo.

Hatua hiyo, imekuja baada ya ziara iliyofanywa na Rais Jakaya Kikwete, nchini Oman Oktoba mwaka jana, ambapo alitoa fursa kwa wawekezaji kuja kuwekeza katika sekta za maendeleo nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam, jana Mwenyekiti wa Kampuni ya Al Hayat Development, Sheikh Salim Al Harthy, alisema hatua ya uwekezaji huo, utasaidia kufungua milango kwa nchi na Watanzania kwa ujumla.

Alisema makubaliano hayo, yamefikiwa na Mtukufu Sultan Qaboos Bin Said Sultan wa Oman. Alisema katika sehemu ya kwanza ya kujitolea kwa nchi hiyo, itaingia makubaliano ya kusaini mkataba maalum kuisaidia ATCL, kwa kuwekeza Dola za Marekani milioni 100 na kuongeza ndege za makampuni mengine. Alisema uwekezaji huo, utakwenda sambamba na ununuzi wa ndege ambazo zitatumika katika safari za ndani na nje ya Afrika.

“Kutokana na ziara ya Rais Jakaya Kikwete katika nchi ya Oman, Oktoba mwaka jana, alifanikiwa kufanya mazungumzo kwa kirefu na Mtukufu Sultan Qaboos Bin Said Sultan, na kukubaliana uamuzi wa kuwekeza nchini.

“Kabla ya makubaliano haya, yalifanyika makongamano mengi nchini Oman, ambayo yalishirikisha makampuni mbalimbali, sasa yameamua kuutumia muungano wao na kufanya uwekezaji mkubwa kwa nchi yetu.

“Uwekezaji huu mkubwa kwa ATCL, utafungua njia za kibiashara kwa kuwa na ndege za kisasa, ambazo zitafanya biashara ya kubeba abiria ndani ya nje ya nchi.

“Tunamshukuru Mtukufu Sultan Qaboos Bin Said wa Oman na Rais Kikwete, kutupatia nafasi hii, hasa ukizingatia kipindi hiki tuna mpango wa kujenga kituo cha mafunzo ya masuala ya ndege kwa ATCL.

“Mbali na hili, tutajenga ofisi ya kisasa ambayo itakuwa kwa ajili ya matumuzi ya shirika hili la ndege ya Tanzania, pamoja na kufanya shughuli nyingine za maendeleo tunazotarajia kuanza ndani ya miezi sita hadi kumi kutoka sasa,” alisema.

Sheikh Salim Al Harthy, alisema uwekezaji huo, ni matokeo mazuri ya mazungumzo kati ya Rais Kikwete na Serikali ya Oman.

Mwaka jana, Rais Kikwete alipotembelea Oman, baada ya kualikwa na Mtukufu Sultan Qaboos Bin Said, ambapo aliambatana na ujumbe wa mawaziri na viongozi waandamizi wa biashara. Katika ziara hiyo, Rais Kikwete alibadilishana uzoefu wa uhusiano na kuangalia namna ya kudumisha ushirikiano wa nchi hizo, kuhusiana na biashara, elimu na utamaduni. Ziara ya Rais Kikwete katika nchi ya Oman ni ya pili kufanyika, baada ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere kutembelea nchi hiyo, mwaka 1985.
Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.