Rais Jakaya Kikwete alitoa ahadi lukuki kwa makundi mbalimbali 
ya jamii katika kipindi cha miaka 10 ya utawala wake kupitia kaulimbiu 
yake ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania, lakini anaondoka madarakani 
mwaka huu akiwa ameshindwa kutekeleza ahadi nyingi  na zaidi ameacha 
manung’uniko na mgawanyiko.
|  | 
| Rais Jakaya Kikwete anaondoka madarakani akiwa ameshindwa kuwatimizia waumini wa Kiislamu ahadi ya kuwaundia Mahakama ya Kadhi. Picha na Maktaba | 
Mwaka 2005, alipoingia madarakani aliahidi kuondoa
 uhasama wa kisiasa kati ya visiwa vya Unguja na Pemba, kuondoa migogoro
 ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, kuwapatia wanahabari Sheria ya 
Habari, kupambana na ufisadi; na mwaka 2010 aliahidi kuwapa Waislamu 
Mahakama ya Kadhi na wananchi Katiba Mpya.
Mambo hayo sita yamekuwa mfupa mgumu kwa Rais 
Kikwete na anaondoka akiacha uhasama mkubwa wa kisiasa visiwani 
Zanzibar, wakulima na wafugaji wakihasimiana, ufisadi ukiotesha mizizi, 
vyombo vya habari kufungiwa, nchi ikipasuka kuhusu Katiba Mpya na 
Mahakama ya Kadhi.
Sheria ya Habari
Rais Kikwete alijigamba kuruhusu uhuru wa vyombo 
vya habari na Serikali yake ilianza kuandaa muswada mwaka 2007 lakini 
haukufikishwa bungeni. Machi 30, 2012 Kikwete alipokuwa mgeni rasmi 
katika utoaji Tuzo za Umahiri katika Uandishi (EJAT), aliahidi mambo 
mengi mazuri likiwamo la kuwasilishwa Muswada wa Sheria ya Kusimamia 
Vyombo vya Habari katika Bunge la Oktoba.
Kuthibitisha kwamba Rais Kikwete hamaanishi 
anachokisema, Julai 30, 2012 yaani miezi minne tangu awape matumaini 
wanahabari, Serikali yake kupitia Idara ya Habari (Maelezo), ililifungia
 gazeti la MwanaHalisi, kwa muda usiojulikana. Halafu Septemba 27, 2013 
gazeti  la Mtanzania lilifungiwa kwa muda wa siku 90 na Mwananchi kwa 
siku 14. Magazeti mengine yaliyowahi kufungiwa siku 90 ni Kulikoni 
(Januari 8, 2010) na MwanaHalisi (Oktoba 13, 2008).
Desemba 8, 2011 mwanasafu wa gazeti la Tanzania 
Daima, Samson Mwigamba; mhariri mtendaji wa gazeti hilo, Absalom Kibanda
 na aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Mwananchi Communications Ltd 
iliyochapisha gazeti hilo walifikishwa kortini wakikabiliwa na mashtaka 
ya uchochezi.
Septemba 2, 2012 aliyekuwa mwandishi wa habari wa 
kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi alipigwa na kufariki dunia akiwa 
mikononi mwa polisi alipokuwa akiripoti mkutano ya Chama cha Demokrasia 
na Maendeleo katika kijiji cha Nyololo Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa. 
Januari 23, 2015 Serikali yake imeamua kupiga marufuku usambazwaji wa 
gazeti la The EastAfrican nchini.
Katiba Mpya
Ilani ya CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 
haikuwa na ahadi ya Katiba Mpya, lakini Novemba 8,      2010 siku 
alipozindua Bunge la 10, Kikwete alizungumzia umuhimu wa kuipa uhai 
Katiba iliyopo na Februari 2011 katika sherehe za CCM alisema atawapa 
Watanzania Katiba Mpya.
Kwa kuwa wazo hilo halikutokana na CCM, Kikwete 
alipata shida kulinadi ndani ya vyombo vya chama na Serikali na hata 
walipokubali, wasaidizi wake walidai ni marekebisho yeye akisema 
kuhuisha. Serikali ikatengeneza Sheria ya Mabadiliko ya Katiba,  akaunda
 Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji mstaafu, Joseph Warioba 
ambayo ilifanya kazi ya kukusanya maoni na kutengeneza Rasimu ya Katiba.
 Mwaka 2014 akaunda Bunge Maalumu la Katiba (BMK) ambalo liliandika 
Katiba Inayopendekezwa.
Ukosoaji mkubwa aliofanya Rais Kikwete alipozindua
 BMK, uliwagawa wabunge katika makundi mawili ya kudumu; wanachama wa 
CCM upande mmoja na wapinzani upande wa pili. Pia, Tume ya Warioba 
ilipingana na BMK lililoongozwa na Samuel Sitta.
Aprili 16, wapinzani chini ya umoja wao Ukawa walisusia BMK, 
likawa pigo la kwanza. Pigo la pili na la mwisho ni Januari 23, 2015 
Ukawa walipotangaza kususia Kura ya Maoni iliyopangwa Aprili 30. 
Kutokana na misuguano hiyo, na kwa kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi 
haikuwa imepewa fedha za kutosha zikiwamo za kununulia mashine za BVR 
kwa ajili ya kuandikisha wapigakura, Aprili 2, 2015 Kura ya Maoni 
ikafutwa hadi itakapotangazwa tena.
Mahakama ya Kadhi
Mwaka 2010, katika mazingira tata CCM iliingiza 
ahadi ya Mahakama ya Kadhi kwenye Ilani ya Uchaguzi. Lakini Serikali 
haikufanya juhudi kubwa kutengeneza mazingira ya kukubalika kwa mahakama
 hiyo; kwanza, kwa Waislamu wenyewe; pili, kwa Wakristo.
Kosa namba moja. Agosti 30, 2011 alipokuwa mgeni 
rasmi katika Baraza la Idi katika msikiti wa Gadaffi, Dodoma, Rais 
Kikwete aliwaambia Waislamu kwamba amezungumza na maaskofu na 
wamemwambia kuwa hawana shida na Mahakama ya Kadhi isipokuwa wanataka 
iundwe na kuhudumiwa na Waislamu wenyewe. Waislamu walilalamika mambo 
yao kujadiliwa kwanza na Wakristo ndipo waelezwe wao.
Kosa namba mbili. Serikali imekuwa ikikutana na 
uwakilishi mpana wa maaskofu kutoka madhehebu yote kupata maoni yao 
lakini imekuwa ikikutana na uongozi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania 
(Bakwata) ambalo halikubaliwi na Waislamu wote.
Kosa namba tatu. Dalili zote zikionyesha hakuna 
uwezekano wa kukubalika kwa Mahakama ya Kadhi, Serikali ilitoa ahadi 
nzito ndani ya BMK na Waislamu waliporidhia, hazikuwepo juhudi za 
kuandaa semina za kuelimisha wadau kuhusu muundo na uendeshwaji wake 
hali iliyosababisha hata baadhi ya Waislamu kuikataa kwamba siyo kati ya
 nguzo tano za Uislamu. Vilevile, lilikuwepo shinikizo kutoka kwa 
maaskofu na hasa ulivyoligawa Taifa mapande mawili.
Mgogoro Zanzibar
Moja ya ahadi nzito iliyofurahiwa na Watanzania ni
 ile ya kumaliza uhasama wa kisiasa Zanzibar kati ya wanachama wa CCM 
wengi wao wakiwa Unguja na wenzao wa Chama cha Wananchi (CUF) ngome yao 
ikiwa Pemba. Ahadi hiyo iliianza kutekelezwa baada ya kuanzishwa 
mazungumzo baina ya viongozi wa CCM na CUF na hatimaye kufikia 
maridhiano na Katiba ikafanyiwa marekebisho kuruhusu Serikali ya 
Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuongozwa kwa mfumo wa Serikali ya Umoja wa 
Kitaifa (SUK).
Pamoja na mafanikio hayo, uhasama wa kisiasa 
umerejea; CCM wakionekana kuwa vinara wa siasa za uhasama; wanawavizia 
na kuwapiga wafuasi wa CUF. Katika mikutano yao huhubiri ubaguzi kwa 
kuzingatia asili ya watu kwamba Wazanzibari wenye asili ya Kiarabu 
wanatajwa kuwa ni vibaraka wenye lengo la kurudisha utawala Kisultani. 
Wanadai kwamba vibaraka hao wanataka kurudisha utawala wa Sultani 
aliyepinduliwa mwaka 1964,  Jamshid bin Abdullah Al Said, kizazi cha 
masultani kutoka Oman kilichotawala Zanzibar kuanzia mwaka 1832 hadi 
mwaka 1964.
Huu ni unafiki, ukweli ni kwamba Jamshid 
aliyetawala Zanzibar kuanzia Julai Mosi, 1963, baada ya kupinduliwa 
Januri 12, 1964 alikimbilia Uingereza. Salmin Amour, Rais wa awamu ya 
tano wa SMZ alitangaza kumpa uhuru Sultani huyo anayeishi Portsmouth, 
kurejea Zanzibar kama raia mwingine. Hajarudi.
Wakulima, wafugaji
Jambo jingine kubwa aliloahidi kushughulikia 
katika hotuba yake ya uzinduzi wa Bunge la Tisa Desemba 31, 2005 ni 
kulinda mazingira kwa kuhakikisha wakulima wanaachana na kilimo cha 
kuhamahama na wafugaji aliodai wanatembea umbali mrefu kusaka malisho 
wakiwa wamekonda na mifugo imekonda, kuwapa mbinu za ufugaji ili sekta 
ya ufugaji iwe ya kisasa.
Baada ya kuunda Serikali alitembelea Wizara ya Maendeleo ya 
Mifugo, aliwaagiza watendaji: kuongeza mchango wa sekta ya mifugo katika
 pato la Taifa; kudhibiti uhamishaji holela wa mifugo; kuimarisha huduma
 za ugani; kufufua ranchi zilizopo na kuhakikisha zinafanya kazi 
iliyokusudiwa; na kutoka katika uchungaji wa kuhamahama na kwenda katika
 ufugaji wa kisasa na wa kibiashara.
Vilevile, aliwaagiza kutafuta masoko ya nje ya 
kuuza mifugo na mazao yake; na kufikisha madawa na huduma za mifugo kwa 
wafugaji. Lakini miongoni mwa picha zilizojaa katika mitandao mbalimbali
 ya kijamii kuanzia mwaka 2006 ni za maiti ya wakulima na wafugaji 
katika maeneo tofauti nchini.
Baadhi zikionyesha watu waliokatwa koo, 
waliopasuliwa vichwa na waliopigwa mishale na mikuki; nyingine 
zikionyesha nyumba au maboma yalivyochomwa moto, mifugo kuuawa. Hasira 
na uhasama vimetanda kila mahali.
Katika kipindi cha uongozi wake, imeshuhudiwa 
migogoro mingi ya ardhi kati ya masikini na matajiri, wakulima wazawa na
 wawekezaji na mbaya zaidi kati ya wakulima na wafugaji ambao 
wamechinjana Mbarali, Kilosa, Kiteto na kwingineko. Rais Kikwete 
anaondoka huku hali ikiwa mbaya kuliko alivyoikuta.
Vita ya ufisadi
Ahadi nyingine ya Rais Kikwete kwa Watanzania 
aliyoitoa katika hotuba yake ya Desemba 31, 2005 ni kuanzishwa kwa 
mapambano dhidi ya rushwa kubwa kubwa kwa vitendo na siyo lazima 
ushahidi uwepo kwa asilimia 100.
Alisema: “hata ukihisiwa umekula rushwa 
tutahakikisha tunachunguza na kushughulikia…” Lakini licha ya Taasisi ya
 Makosa Makubwa ya Jinai ya Uingereza (SFO) kutaja waliokula rushwa 
kupitia ununuzi wa rada ya kuongozea ndege, Serikali ilikataa 
kuwashughulikia.
Mafisadi wengine ambao hawakushughulikiwa na 
Serikali yake ni walionufaika kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (Epa), 
walitoengeneza dili kupitia kampuni ya kufua umeme wa dharura ya 
Richmond/Dowans, walioiuzia vifaa hospitali ya Muhimbili kwa bei mbaya, 
waliochangisha fedha za kula tu baada ya kupitisha Bajeti ya Wizara ya 
Nishati na Madini (2012) na sasa waliotengeneza mazingira ya kuchotwa 
Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow.
Hata hivyo, Serikali imewanasa walimu na mahakimu na kuwafungulia mashtaka kwa madai ya kuchukua rushwa ndogondogo.
Chanzo cha habari na gazeti la kila siku la Mwananchi
Post a Comment