WATU watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wamevamia kituo cha mafuta cha EAFCO kilichopo eneo la Mwenge mjini Singida, na kupora shilingi laki tano baada ya kufyetua risasi moja hewani kwa lengo la kuwaogofya wafanyakazi.


 Watu hao wanadaiwa walikuwa wamebeba bunduki moja ya kienyeji inayodhaniwa kuwa ni aina ya gobore na bastola moja.


 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida,Geofrey Kamwela,alisema tukio hilo limetokea Septemba tisa mwaka huu saa 11.00 jioni eneo la Mwenge mjini Singida.


 Alisema awali watu hao waliteka taksi yenye usajili T.637 AGL aina ya Toyota mark 11 iliyokuwa ikiendeshwa na Ernest Joseph (32) mkazi wa Misuna mjini Singida,na kisha kuitumia katika kutekeleza azma yao.


 “Huyu dereva wa taksi baada ya kutekwa,alifungwa kamba ya katani na kuweka kwenye buti ya nyuma na kwenda naye kwenye eneo la tukio na wakati uporaji huo unafanyika,dereva huyo alikuwa ndani ya buti la gari lake”,alisema Kamwela.


 Kamanda huyo alisema majambazi hayo yalipofika kwenye kituo hicho cha mafuta,walifyetua risasi moja hewani kwa kutumia bunduki aina ya gobore kwa lengo la kuogofya watumishi na wateja waliokuwa kwenye kituo hicho.Baada ya hapo,ndipo yalipofanikiwa kupora shilingi 500,000.


 Alisema polisi walipopata taarifa ya tukio hilo,walifika mara moja kwenye kituo hicho na kukuta majambazi hayo kwa kutumia taski waliyoiteka,waliishatoroka lakini hawakufika mbali walipata ajali na kuitekeleza taksi hiyo na wao kukimbilia kusikojulikana.


 “Wakati majambazi hayo yanatoroka,moja lilidondosha bunduki aina ya gobore ambalo limeokotwa na polisi.Kwa sasa tunaendelea na msako wa kuyasaka majambazi hayo ili sheria iweze kuchukua mkondo wake”alisema Kamwela.


 Wakati huo huo,Kamanda Kamwela alisema dereva Ernest alifikiwa katika hospitali ya mkoa na kupata matibabu na kisha kuruhusiwa.


MWISHO.
Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.