.awaasa vijana kutotumiwa na wanasiasa kwa maslahi yao
.ashangaa wajuzi walivyompachika jina la Ruksa enzi za miaka 1990s 


Rais Mstaafu wa awamu ya pili, Alhaji Ali Hassan Mwinyi amesema kuna baadhi ya watu katika jamii kutumia elimu, ujuzi na maarifa yao kuangamiza, kubomoa na kudumaza ustawi wa jamii kwa maslahi binafsi na si ya umma. Mo blog inaripoti.
Mzee mwinyi amesema hayo leo asubuhi wakati wa kuadhimisha siku ya Kimataifa ya amani duniani inayoadhimishwa 21th Septemba kila mwaka katika ukumbi wa Don Bosco jijini Dar es Salaam, amesema kuna baadhi ya watu wanatumia elimu yao vibaya kwa kupanga kuua watu wengine kwa maslahi yao aidha ya kisiasa au ya kiuchumi.

“Elimu kwa kawaida kuleta matokeo mazuri kwa jamii husika endapo itatumika sawia kwa malengo yaliyokusudiwa na kwa maendeleo endelevu ya taifa kwa ujumla, ila kuna baadhi ya wanajamii kutumia ujuzi huu vibaya na kuangamiza ustawi wa jamii husika,” amesema. 

Mzee Mwinyi aliendelea kusema kwamba katika kuadhimisha siku ya kimataifa ya amani duniani yenye kauli mbiu “education for peace” ni lazima elimu kwa ajili ya amani iwe endelevu hapa duniani ili iweze kuleta suluhu na utengamano katika jamii na mataifa yote duniani.

Amesema kwamba vijana nchini lazima waepuke kutumiwa na wanasiasa kwa maslahi yao ya kisiasa na wajifunze kutatua matatizo yao kwa njia ya amani bila ya kuwa na mihemko, jazba, misongo na hasira ili kuendelea kudumisha amani na upendo katika nchi yetu ambayo ni kisiwa cha amani.

“nawaasa vijana wakitanzania wa leo hata kama mmenyimwa haki zenu ni bora kutumia njia ya kistaarabu na kutumia elimu mnayopata mashuleni bila kusahau macho, masikio na vipawa vyenu mlivyopewa na mwenyezi mungu katika kutafuta haki yenu kwa njia ya amani bila misukosuko,” aliongeza.

Mzee Mwinyi alitumia nafasi hiyo kuwashangaa baadhi ya watu kwa kutumia ujuzi na elimu yao kwa kumpachika jina la Ruksa bila yeye kujua wametumia muktha gani kumpa jina hilo, lakini Mzee Mwinyi alitumia jukwaa hilo pia kuwapa ruksa vijana kutumia elimu yao kuleta hali ya amani na utulivu ndani ya nchi.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) Jama Gulaid amesema kwamba Umoja wa Mataifa uliweka maazimio siku ya kimataifa ya amani duniani ili watu wanaogombana na kupigana kwa shida mbalimbali kupata nafasi ya kuweka silaha zao chini katika siku hii adhimu.

Amesema kupitia azimio hilo ambalo lilizinduliwa mwaka 1982 kwa mara kwanza linatambua uwepo wa watu wanaoathirika na vita katika sehemu mbalimbali duniani na waliokwishapoteza maisha kutokana na matatizo vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Naye Mratibu na Mtathimini wa Mtandao wa watoto na vijana kutoka Imani Mbalimbali (GNRC) Bi, Joyce Mdachi amesema swala la amani na utulivu linaanzia kwenye kaya hadi ngazi ya taifa kwahiyo ni muhimu kwa jamii na vijana kuelewa amani inaanzia nyumbani.

“jamii iliyolelewa katika mazingira mazuri ina nafasi kubwa ya kuleta matokeo chanya kwenye mustakabali wa taifa kwa ujumla lakini jamii iliyolelewa vibaya haiwezi kubadilisha taifa kwa sababu ni zao la tunda baya,” alisema.

Mdachi alisisitiza kwamba kuporomoka kwa maadili ndani ya jamii ya leo swala hilo pia lilianzia kwenye kaya ya mtu mmoja mmoja hadi ngazi ya taifa ambapo leo hii taifa linashuhudia mambo ya kifisadi, rushwa na ubadhilifu wa mali za umma kunakofanywa na viongozi waandamizi.

Mwisho
 


Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.