NDOA nyingi za utotoni husababishwa na tabia ya baadhi ya wazazi na walezi kuwalazimisha watoto wao wa kike kuolewa katika umri mdogo kwa tamaa ya kujipatia fedha ama utajiri katika familia zao jambo ambalo linawanyima haki ya kusoma watoto wengi kwani watoto hawa wanakuwa wako katika umri chini ya miaka kumi na nane.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Mtaa wa Wailesi Wilaya ya Temeke Bw. Abdul Kidege wakati wa ufunguzi wa Tamasha la Jamvi la Vijana linalofanyika kila mwisho wa mwezi katika kituo cha vijana UMATI jijini Dar es Salaam.

Bw. Kidege amesema kuwa kuna baadhi ya wazee na vijana wenye tabia ya kuwarubuni wasichana wadogo kwa kuwapa pesa na vitu vya thamani kwa lengo la kuwashawishi kuolewa nao na pia kuna baadhi ya wazazi ambao wakati mwingine ushirikiana katika kufanikisha azma hiyo jambo ambalo ni kinyume na haki za watoto katika jamii.

“Kuna baadhi ya wasichana wenye umri mdogo wamekuwa wakinyanyaswa kijinsia kwa kubakwa na wengine kulazimishwa na wazazi wao wenyewe kuolewa na watu wazima ambao wamewazidi umri, jambo hili halikubariki na vijana nawaasa msikubali kurubuniwa kwa pesa au vitu toka kwa watu wa namna hiyo”. Alisema Bw. Kidege.

Kwa upande wake Afisa Vijana Msaidizi Chama cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania (UMATI) Bi. Upendo Daud amewaeleza vijana waliohudhuria tamasha hilo kuwa vijana wanapohudhuria matamasha katika kituo cha UMATI wanapata fursa kubwa ya kupata elimu bure juu ya afya ya uzazi, athari za mimba za utotoni, kupima Ukimwi, ushauri nasaha, uzazi wa mpango pamoja na uelimishaji rika jambo ambalo linawafanya vijana wengi waweze kujitambua na kujikinga.

 “Hili ni Tamasha kwaajili ya vijana linaloandaliwa kila mwisho wa mwezi na Youth Action Movement (YAM) kwa lengo la kuwaelemisha vijana juu ya mambo mbalimbali yanayohusiana na afya na mada kuu ya tamasha hili kwa leo ni Ndoa za umri mdogo  na athari zake”. Alisema Bi. Upendo.

Youth Action Movement (YAM) ni kikundi cha Vijana ambacho kilianzishwa na chama cha uzazi na malezi bora Tanzania (UMATI) kwa ufadhili wa Internationa Planned Parenthood Federation (IPPF). Chama hiki cha vijana kinapatikana katika kila tawi la UMATI nchi nzima na kwa tawi la Dar es Salaam ndiyo waandaaji wa Jamvi la vijana kila mwezi ambapo husaidia kutoa huduma bure kwa vijana kuhusu afya ya uzazi, kupima Ukimwi, ushauri nasaha, uzazi wa mpango pamoja na uelimishaji rika.




Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.