Wakazi wa mjini Dodoma wakiwa kwenye ibada maalumu ya kushukuru kumalizika salama na amani kwa mchakato wa kupatikana kwa Katiba inayopendekezwa, ibada iliyofanyika kwenye Viwanja vya Nyerere Square,jana.  Picha na Edwin Mjwahuzi

Dar/Zanzibar. Katiba inayopendekezwa itakutana na kihunzi kingine katika utekelezwaji wake kutokana na Zanzibar kutakiwa kubadili Katiba yake, zikiwamo ibara zilizobeba msingi wa mabadiliko ya 10 katika Katiba ya Zanzibar.
Mabadiliko hayo ya mwaka 2010, kwa kiasi kikubwa yanakinzana na Katiba ya sasa ya Muungano pamoja na Katiba inayopendekezwa ambayo inakabidhiwa leo kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein mjini Dodoma.
Ili Katiba inayopendekezwa iweze kutekelezeka ni lazima Zanzibar ifanyie mabadiliko Katiba yake kwa kuwa Katiba ya Muungano ndiyo Sheria Kuu.
Hata hivyo, wachambuzi wanahoji iwapo mabadiliko hayo yatawezekana kirahisi kwa kuwa yanatakiwa kuidhinishwa kwa kura ya maoni ya wananchi wa Zanzibar, baada ya kupita kwenye chungu cha Baraza la Wawakilishi na kuamuliwa kwa theluthi mbili za kura.
Tofauti zilizopo
Mosi, Katiba ya Zanzibar inatamka kwamba Zanzibar ni nchi ambayo eneo la mipaka yake ni lote la visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na visiwa vidogo vilivyoizunguka na bahari yake ambayo kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ikiitwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar.

Ibara ya pili inaitambua Zanzibar kuwa miongoni mwa nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Masharti hayo ni kinyume na Katiba inayopendekezwa ambayo katika ibara yake ya kwanza inatamka kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi yenye mamlaka kamili ambayo imetokana na Muungano wa nchi mbili za Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambazo kabla ya Hati ya Makubaliano ya Muungano ya tarehe 22 Aprili, 1964 zilikuwa nchi huru.
Pili, Katiba ya Zanzibar katika Ibara ya 26 inatamka kwamba Rais wa Zanzibar ni Mkuu wa nchi ya Zanzibar, jambo ambalo ni kinyume na Katiba inayopendekezwa katika Ibara ya 80 (2) ikisema; Rais wa Jamhuri ya Muungano atakuwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Amiri Jeshi Mkuu.
Tatu, Katiba ya Zanzibar katika Ibara ya pili A inatamka kwamba kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali, Rais anaweza kuigawa Zanzibar katika mikoa, wilaya na maeneo mengineyo kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.
Masharti hayo ni kinyume cha Katiba inayopendekezwa Ibara ya 2(2) ambayo inatamka: “Rais wa Jamhuri ya Muungano atakuwa na mamlaka ya kuigawa Jamhuri ya Muungano katika mikoa, wilaya na maeneo mengine, isipokuwa kwa upande wa Tanzania Zanzibar, Rais atashauriana na Rais wa Zanzibar kabla ya kuigawa Tanzania Zanzibar katika mikoa, wilaya au maeneo mengine.

Nne, Katiba ya Zanzibar katika Sura ya 3 Ibara ya 24(3) inasema: “Rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama Kuu (Zanzibar) katika shauri lililofunguliwa dhidi ya masharti ya Sura hii ya Katiba yatasikilizwa na Mahakama Kuu (Zanzibar) mbele ya majaji watatu bila ya kumjumuisha Jaji aliyeamua shauri hilo mara ya kwanza.
Majaji hao watatu watateuliwa na Jaji Mkuu na uamuzi wao utakuwa ni wa mwisho na hautokatiwa rufaa kwenye Mahakama ya Rufaa ya Tanzania.
Masharti hayo ni kinyume na Katiba inayopendekezwa Ibara ya 167(1)(2) na(3) ambazo zinatamka kwamba: “(1) Kutakuwa na Mahakama ya Jamhuri ya Muungano, (2) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Katiba hii na sheria nyingine yoyote, itatekeleza mamlaka yake kupitia Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani na (3) Mahakama ya Jamhuri ya Muungano itakuwa ni chombo chenye mamlaka ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano.
Mahakama ya Juu na Rufani ndiyo zenye Mamlaka ya juu ya kutoa haki nchini na uamuzi wake ni wa mwisho.
Sita, kuhusu masharti ya fedha yahusuyo SMZ ambayo Katiba ya Zanzibar Ibara ya 104(1) inasema: “Kutakuwa na mfuko mkuu wa hazina ambao bila ya kuathiri sheria nyingine yoyote inayotumika, zitawekwa fedha zote zitakazopatikana kutokana na njia mbalimbali kwa ajili ya matumizi ya SMZ.

Hata hivyo, Katiba inayopendekezwa katika Ibara ya 251 inasema: “Serikali ya Jamhuri ya Muungano itatunza akaunti maalumu itakayoitwa “Akaunti ya Fedha ya Pamoja” na ambayo itakuwa ni sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambamo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili kwa kiasi kitakachoamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa sheria itakayotungwa na Bunge, kwa madhumuni ya shughuli za Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano.
Maoni ya wadau
Kutokana na mgongano huo, wanasheria, wanasiasa na wananchi wa Zanzibar wametoa maoni tofauti; baadhi wakieleza kuwa iwapo itapitishwa kuna hatari ya kuibuka mgogoro wa kikatiba baina ya pande mbili za Muungano.
Akizungumzia tofauti hizo, Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alisema ingawa Katiba inayopendekezwa imetaja mambo kadhaa mazuri, utekelezaji wake unategemea zaidi mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar na ina maswali mengi kuliko majibu hasa kuhusu muungano na mgombea binafsi.
Alisema licha ya Zanzibar kuridhia mambo kadhaa kuwekwa katika orodha ya mambo ya Muungano, hali inaweza kuwa tofauti ukifikia wakati wa Zanzibar kubadili Katiba yao ili kuwezesha utekelezaji wa mabadiliko hayo.
Pia, aligusia suala la kodi ya mapato, ushuru wa forodha na bidhaa kuwa mambo ya Muungano na kufafanua kuwa kwa mabadiliko hayo, Zanzibar itashindwa kutekeleza mambo mengi licha ya kupewa uwezo wa kusimamia mambo yake, kwa sababu mapato yake yanaingia kwenye mfuko wa mapato ya muungano.

Mwakilishi wa Mji Mkongwe (CUF), Ismail Jussa alisema msimamo wa Zanzibar umeshahitimishwa na Mwanasheria Mkuu wake, Othman Masoud Othman wakati alipopiga kura ya ‘hapana’ kwa mambo yanayohusu Muungano.
“Hatuko tayari kufanya marekebisho na ikitokea labda kuongeza mamlaka zaidi kwa Wazanzibari.”
Mbunge wa Uzini (CCM), Muhammed Seif Khatib alisema kwa kifupi, “Sina majibu kwa hilo, siwezi kujibu kwa kipindi hiki.”
Mbunge wa Tumbatu (CCM), Juma Othman Ali alisema: “Rasimu inayopendekezwa haina tatizo na itapita kwani hakuna tatizo lolote na wananchi hawana sababu ya kutoipitisha.”
Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Zanzibar), Vuai Ali Vuai alisema mchakato wa Katiba unakwenda hatua kwa hatua na jambo ambalo lipo mbele ni kuipitisha Katiba inayopendekezwa kisha itafuatiwa na kuibadili Katiba ya Zanzibar.
“Hatua ya kwanza ni kuipitisha Rasimu kuwa Katiba na ili ipite ni lazima ipitishwe na Wazanzibari na kama ndiyo hivyo wameipitisha hiyo, hata Katiba nayo watakubali kuifanyia marekebisho kulingana na masharti,” alisema.
Kuhusu kura ya hapana ya Mwanasheria Mkuu, Vuai alisema, “Kura yake moja ni ndogo sana, kuna kura zaidi ya 150 zilipigwa pale bungeni, moja haiwezi kuharibu chochote katika huu mchakato, alipiga kadri alivyoona inafaa na sioni kama ni shida.”

Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar, Awadhi Ali Said alisema kabla ya kufanyika marekebisho hayo, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), watalazimika kupiga kura kupitisha muswada wa marekebisho ya Katiba kwa mujibu wa Kifungu cha 4 na 80 cha Katiba yake na lazima theluthi mbili ipatikane.
Alisema baada kupitishwa na Baraza hilo ndipo SMZ inaweza kuitisha kura ya maoni kwa wananchi lakini iwapo hatua ya awali itakwama wakati Rasimu ya Katiba ya Muungano imepitishwa, mgogoro mkubwa wa kikatiba utaibuka.
Mwanasheria Mkuu wa zamani (SMZ), Hamid Mbwezeleni alisema suala la Katiba ya Zanzibar kufanyiwa marekebisho hakuna mjadala iwapo Katiba inayopendekezwa itapitishwa.
Alisema kuwa Katiba ya Muungano ndiyo Katiba mama hivyo vifungu vya katiba ya Zanzibar vinavyogongana na ile ya Muungano vitalazimika kufutwa.
Mbwezeleni alisema marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar yanawanyima haki wananchi ya kutumia Mahakama za juu za rufaa.


“Kama tunakubali Muungano tukubali na mambo mengine, suala la Katiba ya Zanzibar kufanyiwa marekebisho halikwepeki katika mazingira ya Serikali mbili,” alisema.
Katibu wa Bavicha Zanzibar, Francis Warema alisema mgogoro wa kikatiba unanukia kwa vile hakuna Mzanzibari atakayekubali Zanzibar kuondolewa hadhi yake ya kuwa ni nchi.
Mkazi wa Mwembemakumbi, Masoud Othman Said (49) alisema muda wa kufanya marekebisho ya Katiba ya Zanzibar upo, jambo la msingi lazima iwepo nia njema.
Alisema kinadharia, Katiba ya Zanzibar imetoa hadhi ya Zanzibar kuwa nchi lakini kivitendo huwezi kuwa na nchi bila ya kuwa na uraia, ulinzi, sarafu, ardhi pamoja na sifa za kujiunga na jumuiya za kimataifa ikiwamo Umoja wa Mataifa.
Imeandikwa na Fidelis Butahe, Ibrahim Yamola na Mwinyi Sadallah

Chanzo cha habari na gazeti huru la kila siku la www.mwananchi.co.tz















































































Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.