Matokeo mabovu --pengine-- kuliko yote ya Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne kuwahi kutokea katika historia ya taifa la Tanzania yamezua balaa la aina yake baada ya wanafunzi wawili kujiua kwa kujipiga vitanzi hadi kufa.

Taarifa zilizothibitishwa leo na jeshi la Polisi zimeeleza kuwa wanafunzi waliojiua kutokana na matokeo hayo ni wa jijini Dar es Salaam na mwingine kutoka mkoa wa Tabora.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora,  Anthony Rutta, amesema leo kuwa mhitimu aliyejiua mkoani humo ni  Michael Fidelis (19) mkazi wa Mtaa wa Mwinyi, Kata ya Chemichemi aliyemaliza katika Shule ya Sekondari ya Kanyenye mjini Tabora.

Kamanda Rutta amesema kuwa Fidelis amejiua kwa kujinyonga hadi kufa baada ya kwenda kuangalia matokeo juzi Jumatatu (Februari 18, 2012), saa 11:00  jioni. Baadaye akakutwa amejinyonga chumbani kwake kwa kutumia kamba ya manila, kisa ikiwa ni kupada divisheni ziro.

Taarifa kutoka kwa rafiki wa kijana huyo ambaye maziko yake yalifanyika juzi, zilisema awali alipigiwa simu na kaka yake aishiye Mbeya kumwambia kwamba matokeo yametoka.

Walisema wakiwa kwenye intaneti, kijana huyo ambaye ni wa kwanza kuzaliwa kwa mamake, alionekana amenyong’onyea, “Aliporudi nyumbani alinyong’onyea zaidi. Hakusema chochote. Kumbe alipotoka hapo alikwenda kujinyonga,” alisema mmoja wa watu waliokuwa naye.

Sehemu ya ujumbe alioacha marehemu Fidelis ulisomeka hivi: “Nisamehe sana mama, usitafute mchawi... nakupenda sana. Uamuzi niliouchukua ni sababu ya matokeo mabaya, nakutakia maisha mema.

Matokeo ya shule ya Kanyenye yanaonyesha kuwa wahitimu 85 walipata sifuri na hakuna aliyefaulu kwa daraja la kwanza wala la pili.

Kwa mujibu wa ndugu zake, kijana huyo alikuwa akiishi na ndugu zake nyumba tofauti na mama yake ambaye alishaachana na baba yake mzazi na kuolewa na mume mwingine.  Ilielezwa kuwa alikuwa na kawaida ya kula usiku nyumbani kwa mama yake. Lakini usiku huo hakuonekana na ilipofika saa 3 usiku walikwenda na kukuta amejifungia ndani wakavunja mlango na kukuta amekufa.

Jijini Dar es Salaam, aliyejiua kwa kujipiga kitanzi baada ya kufeli ni aliyekuwa mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Debrabant iliyopo Mbagala, wilayani Temeke, Barnabas Venant (18).

Kamanda wa Engelbert Kiondo wa mkoa wa kipolisi Temeke, amesema leo kuwa Vicent alikuwa akiishi Nzasa na amejinyonga kwa manila akiwa ndani ya stoo ya nyumba yao juzi saa 10:00 jioni baada ya kuambulia daraja la nne (Div IV), kinyume kabisa na matarajio yake.
Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.