Bunge la Katiba, linaendelea na vikao vyake mjini Dodoma na miongoni mwa hoja kuu katika mijadala yake ni suala la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
 
 Hoja hii ya Muungano, imekuwa na umuhimu wa kipekee na hii ndiyo sababu katika ufunguzi wa Bunge hilo, Rais Jakaya Kikwete alitumia zaidi ya saa moja kuizungumzia.
Salum Rashid

 Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, wakati akiwasilisha Rasimu ya Pili bungeni, pia alitumia zaidi ya saa moja kuzungumzia mambo yanayohusu muungano.

Umuhimu wa suala hilo ndiyo unaofanya mjadala wa Muungano kuwa wa aina yake katika Bunge la Katiba na kufanya watu wengi waufuatilie.

Kutokana na mvutano huu, gazeti hili limefanya mahojiano maalumu na aliyekuwa Katibu wa Baraza la Mapinduzi mwaka 1964, Salum Rashid ili kupata ufafanuzi wake juu ya jambo hilo hasa baada ya Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa kueleza anayojua kuhusu suala hilo.

Swali: Salum Rashid (72) wewe ndiye ulikuwa Katibu wa Baraza la Mapinduzi mwaka 1964. Je, unauzungumzia vipi Muungano?

Jibu: Muungano ni jambo bora, tumekuwa nao kwa miaka 50 sasa lakini una changamoto nyingi ambazo baadhi tangu ulipoanza tuliziona.

Swali: Ni changamoto zipi hizo ambazo tangu mwanzo, zilionekana?

Jibu: Kuna mengi, lakini kikubwa ilikuwa ni usiri wa jambo hili, kwani mimi kama Katibu wa Baraza la Mapinduzi sikujua ila hili la Zanzibar kumezwa tangu wakati huo lilionekana.

Swali: Je, kidogo una ufahamu ilipo Hati ya Muungano? Kuna ambao wanasema ipo Umoja wa Mataifa, wewe unasemaje kwani ulikuwa kiongozi wa Serikali wakati huo?

Jibu: Ninachokumbuka ni kwamba hati haikupelekwa Umoja wa Mataifa (UN), bali kilichopelekwa ni taarifa ya ya kuungana Tanganyika na Zanzibar.

Swali: Katika Bunge linaloendelea sasa kuna mijadala mingi imeibuka kuhusiana na hati ya sheria ya Zanzibar kuridhia Muungano je, una taarifa gani juu ya hati hii?

Jibu: Hati ya Sheria ya Zanzibar Presidential Decree kukubali Muungano, hiyo haipo na wala wasihangaike kuitafuta.

Swali: Kuna hati ya sheria namba 22 ya mwaka 1964, ilisainiwa kwa upande wa Tanganyika na Rais wa Tanganyika wakati huo, Hayati Julius Nyerere, Katibu wa Bunge Pius Msekwa na Spika wa Bunge hilo, Adam Sapi Mkwawa, Aprili 25 mwaka 1964. Je, kwa upande wa Zanzibar hamkupata hati hii?

Jibu: Mimi kama Katibu wa Baraza sijawahi kuiona hiyo Sheria (Presidential Decree) ambayo ilipaswa kusainiwa na Rais wa Zanzibar hayati Abeid Karume na mimi.

Mimi ndiye nilikuwa Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Baraza halikuwahi kuridhia Muungano, kilichofanyika ni kupewa taarifa tu .

Alifafanua kuwa ilipaswa sheria hiyo, kupelekwa rasmi katika Baraza la Mapinduzi na Baraza la Mawaziri lakini haikuwahi kufanyika hivyo.

Swali: Je, unadhani ni kwa nini sheria hii haijasainiwa na wewe?

Jibu: Unajua haya mambo yalikuwa siri sana na kuna mambo mengi yanapotoshwa kuhusu muungano..
Swali: Je, hujawahi kuona Hati ya Muungano na wewe ulikuwa kiongozi mkubwa wa serikali wakati huo?

Jibu: Mimi niliona ile draft (rasimu) ya kwanza ya muungano na nilipoiona nikiwa na hayati Karume nilimshauri vitu vingi na tulirekebisha na baadaye ilirudi Dar es Salaam.

Swali: Je, baada ya kukamilika uliwahi kuiona tena?

Jibu: Hapana, sijaiona nilikuwapo Zanzibar wakati huo, lakini jambo hili baadaye lilifanywa siri kubwa sana, Nyerere hakutaka mtu yeyote ajue na upande wetu Zanzibar hatukupata ushauri wa kisheria hata Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar alikuwa hana taarifa, lakini Tanganyika walikuwa na ushauri wa kisheria.

Swali: Sasa baada ya Miaka 50 ya Muungano, nini maoni yako?

Jibu: Mimi nawataka wajumbe waachane na haya mambo ya hati kwani yamepita na kwa kuwa sote tunautaka Muungano ni muhimu tu kuuboresha.

Swali: Je, unadhani muundo upi unafaa?

Jibu: Mimi ni muumini wa Muungano wa Mkataba, lakini kutokana na mapendekezo mazuri ya Tume ya Jaji Warioba naamini muundo wa Serikali tatu ndiyo mwafaka.

Swali: Lakini kuna hofu ya muungano wa Serikali tatu utavunja Muungano wewe huoni hofu hiyo itatimia.

Jibu: Hakuna sababu ya kuwa na hofu yoyote ya kuvunjika Muungano, kama ambavyo inaelezwa na baadhi ya wanasiasa kwani Muungano wetu siyo wa wanasiasa au Serikali, ni watu. Hapa Zanzibar kuna watu kutoka maeneo mbalimbali ya bara na huko bara wapo Wazanzibar sasa muungano huu hauwezi kuvunjika kirahisi.

Hao wanadhani Tanganyika itakuja kuwa na nguvu zaidi na hivyo kuja kuathiri Muungano hilo haliwezi kutokea kutokana na Muundo uliopendekezwa na Tume ya Warioba.

Swali: Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamekuwa wakipendekeza serikali mbili nini maoni yako.

Jibu: Binafsi najua hasa huku Zanzibar watu hawataki serikali mbili na kama ikilazimishwa na mwakani ni uchaguzi CCM inaweza kupata shida sana kwani asilimia 60 wa Wazanzibariwanataka serikali tatu.


 Chanzo cha habari na gazeti la kila siku la mwananachi 13/04/2014




































































Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.