NCHI za Afrika Mashariki Tanzania zimehimizwa kuiga mfano wa Kenya katika kuweka Sera na Sheria kali ya kudhibiti unywaji mbaya wa pombe wenye madhara makubwa kwa familia na taifa.
Ushauri huo umetolewa na Wajumbe Washiriki wa Mkutano wa Tatu wa Kimataifa kuhusu pombe katika Kanda ya Afrika Mashariki wenye mada kuu ‘pombe ni tatizo chukua hatua sasa’ wametoa ushauri huo mjini Arusha baada ya kuelezwa mafanikio ambayo Kenya imepata kutokana na sheria ya kudhibiti unywaji pombe iliyopitishwa na Bunge la nchi hiyo mwaka 2010.
Mkurugenzi mkuu wa TAMWA, Ananiliea Nkya

Mambo yaliyozingatiwa katika sheria hiyo ya Kenya ni pamoja na kudhibiti usalama na ubora wa viwango vya kilevi kwenye pombe na unywaji holela. Sheria hiyo inapiga marufuku utengenezaji wa pombe kwa kutumia vitu haramu kama vile kemikali ya methanol, mitishamba na kinyesi cha wanyama.
Kwa mujibu wa sheria hiyo mtu akipatikana na hatia ya kutengeneza pombe kwa kutumia vitu hivyo hatari vya kuongeza kiwango cha ulevi adhabu yake ni kifungo jela miaka mitano na faini ya shilingi milioni 10 za Kenya ambazo ni sawa na shilingi milioni 170 za Tanzania au adhabu zote mbili.

Kuhusu kudhibiti unywaji pombe holela, sheria hiyo ya Kenya, tofauti na hapo awali, maalum hivi sasa ni kuanzia saa 11 jioni hadi saa tano usiku. Kadhalika inapiga marufuku watoto kwenda baa au kunywa pombe.Mtu akipatikana na hatia ya kukiuka taratibu za unywaji adhabu yake ni kifungo cha miaka miwili hadi mitano jela au faini ya shilingi 100,000 za Kenya ambazo ni sawa na shilingi milioni moja na laki saba za Tanzania au vyote viwili.

Mwandishi wa TAMWA anayehudhuria mkutano huo amemnukuu Afisa Mtendaji Mkuu wa taasisi ya Serikali iliyopewa mamlaka ya kuratibu utekelezaji wa vifungu vya sheria hiyo (NACADA), Dakta William Okedi akisema utekelezaji wa sheria hiyo umekuwa na mafanikio makubwa.
Dakta Okedi amesema sheria hiyo ya kudhibiti ulevi nchini Kenya imekuwa na mafanikio kwa sababu kabla ya kutungwa kulifanyika utafiti ambao ulibaini kuwa pombe nyingi za kienyeji zinatengenezwa kwa kutumia vitu ambavyo ni hatari kwa maisha ya binadamu.

Mafanikio hayo ni kufungwa kwa karibu nusu ya vilabu vya pombe, kupungua kwa idadi ya vijana wenye umri mdogo wanaokunywa pombe na kuongezeka kwa uzalishaji kutokana na watu kutumia muda mwingi kufanya kazi badala ya kulewa pombe.

Akitoa ushuhuda kuhusu mafanikio ya sheria hiyo, Mbunge John Mututho alisema eneo la Kahuno Murang’a Central Kenya wakulima wa kahawa kwa muda wa miaka kumi mfululizo walikuwa wanapata tani za Kimarekani 57 kwa mwaka lakini katika kipindi cha mwaka 2011/2012 wamepata tani 178 katika ukubwa wa ardhi ile ile ambayo wanalima.

Mbunge huyo ambaye ndiye aliyepeleka Muswada binafsi bungeni ambao uliwezesha kutungwa kwa sheria hiyo amesema utafiti umeonyesha pia kwamba viwanda vya pombe Kenya vimeongeza faida kwa wastani wa asilimia 24 kwa sababu watu wengi wameacha kunywa pombe haramu badala yake wanakunywa bia.
Kadhalika amesema familia zimepata amani na maendeleo kwa sababu wanaume wengi tofauti na zamani ambapo walikuwa wanakesha vilabuni, sasa wanarejea nyumbani mapema .Vile vile makosa ya jinai kama vile ubakaji na mauaji yamepungua kwa zaidi ya asilimia 50.

Mututho ambaye ni mbunge wa jimbo la Naivasha nchini Kenya amesema sheria hiyo inakusudiwa kurejeshwa tena bungeni Septemba 26, 2012 ili kuongezewa makali kupiga marufuku unywaji pombe siku mbili kabla ya siku ya uchaguzi na siku moja baada ya uchaguzi kuzuia ulevi wa pombe kuharibu uchaguzi. Nchi za Afrika Mashariki zinajumuisha Burundi, Rwanda, Uganda, Kenya na Tanzania.

*Habari hii ni Kwa Hisani ya TAMWA
Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.