AJIRA KWA VIJANA ZAATHIRIWA NA UKUAJI MDOGO
WA UCHUMI ULIMWENGUNI
Ripoti mpya ya ILO inayohusu Hali ya Ajira kwa vijana Ulimwenguni – 2013 imeeleza kuwa athari hizi za muda mrefu za tatizo kubwa la ajira kwa vijana zitaendelea kuwapo kwa miongo mingi na hivyo kukiweka kizazi hiki kwenye hatari kubwa ya kutokuwa kwenye kazi zenye staha kwa kipindi chote cha maisha yao.
Pamoja na tofauti zilizopo katika mabara mbalimbali, kiwango cha ajira kwa vijana ulimwenguni kinaendelea kukua na kinategemewa kufikia asilimia 12.8 ifikapo mwaka 2018 – hivyo kuondoa mafanikio yote yaliyopatikana kutokana na kupambana na mproromoko wa uchumi duniani.

Linaloogopesha zaidi ni swala la ukosefu wa ajira kuendelea kuwepo, kuwepo kwa ajira za muda mfupi na kukatishwa tamaa kwa vijana hasa katika nchi zilizoendelea, na pia ajira za kiwango cha chini na zisizo rasmi hasa kwa nchi zinazoendelea.

Kutokana na ripori hii, inakadiriwa kuwa vijana wapatao milioni 73.4 (asilimia 12.6) hawatakuwa na ajira mwaka huu ukilinganisha na asilimia 12.4 mwaka 2012, kiwango karibu sawa na kile cha mwaka 2009 tulipokuwa kwenye kilele cha mporomoko wa uchumi duniani.  Hili ni ongezeko la vijana milioni 3.5 kati ya mwaka 2007 na 2013.

“Viwango hivi vinatuhimiza kulenga sera zetu kwenye kukuza uchumi zaidi, kuboresha mifumo ya elimu na mafunzo, na kuwa na shughuli zinazotoa kipaumbele kwenye kukuza ajira za vijana” kama ilivyosemwa na Jose Manuel Salazar-Xirinachs, Mkurugenzi Msaidizi wa ILO, kuhusu Sera.  Pia ameongeza kuwa “ Makundi haya, Waajiri, wale wanaotoa elimu na vijana mara nyingi hawashirikiani katika jambo hili; kufanya kazi kwa pamoja kwa wadau hawa na kushirikiana kwa karibu ndio kutakakoleta mafanikio”.

Hali katika mabara ulimwenguni
Kiwango kikubwa zaidi cha kukosekana kwa ajira kimekuwepo kwenye eneo la Mashariki ya Kati (Middle East), yaani asilimia 28.3, ikiwa ni zaidi ya robo ya idadi ya vijana wanaostahili kuajiriwa.  Kiwango hiki kinategemewa  kufikia asilimia 30 ifikapo mwaka 2018.  Afrika ya Kaskazini pia ina kiwango kikubwa kinachofikia asilimia 23.7

Vijana wa kike ndio waathirika wakubwa katika maeneo haya – asilimia 42.6 kwa mashariki ya kati na asilimia 37 kwa Afrika ya Kaskazini.

Waliokuwa na kiwango cha chini cha kukosekana kwa ajira mwaka 2012 ni Asia ya Mashariki (asilimia 9.5) na Asia ya kusini (asilimia 9.3).

Matarajio ya baadaye
Kwa nchi zilizoendelea, kiwango cha kukosekana kwa ajira kwa vijana kwa mwaka 2012 kilikuwa asilimia 18.1 na kinategemewa kuendelea kubaki kuwa zaidi ya asilimia 17 hadi kufikia mwaka 2015/16.  Kwa nchi za Greece na Spain zaidi ya asilimia 50 ya vijana hawana ajira.
Vijana wengi wamekatishwa tamaa na swala la kutafuta ajira.  Kwa mfano katika nchi zilizoendelea kwa ujumla vijana waliokata tamaa na wale wasio na ajira walifikia idadi ya milioni 13 kwa mwaka 2012.

Kupungua kwa fursa
Vijana wengi wanalazimika kutochagua kazi – hufanya kazi za muda maalum au zile za masaa ili kujipatia kipato.  Bwana Salazar anaeleza kuwa, “Ajira za kudumu na za uhakika lilikuwa jambo la kawaida kwa vizazi vilivyopita na hali hiyo imebadilika kwa vijana wa sasa.  Kutokana na kuongezeka kwa ajira za muda maalum na zile za masaa tangu mgogoro wa uchumi ulipotokea, inaonyesha kuwa hiyo ndiyo aina ya ajira pekee iliyopo kwa wafanyakazi vijana”.
Taarifa hii inaonyesha pia kuwa kuwepo kwa tatizo hili la ajira kwa muda mrefu kunaleta athari nyingi zikiwemo – kupungua kwa uzoefu wao kwenye kazi na kupotea kwa ujuzi walio nao katika nyanja mbalimbali;  Pia tatizo hili huwafanya vijana kuendelea kukata tamaa ya kupata ajira na/au kipato kwa muda mrefu.

Kuoanisha ujuzi na aina ya ajira
Kutooanisha ujuzi na aina ya ajira pia kunaongezeka.  Hali hii ni ya hatari hasa kama hapatakuwepo na sera za kuwanedeleza kiujuzi vijana wanaotaka kuajiriwa.  Waathirika zaidi katika hali hii ni pamoja na wasichana na wale ambao wapo tayari kwenye  tatizo la kutoajiriwa.

Athari hizi zitaendelea kuongezeka endapo tatizo la ajira kwa vijana litaendelea kuwepo, na litaongeza gharama kiuchumi na kijamii – yaani kuongezeka kwa umaskini na ukuaji finyu wa uchumi.

Hatua zenye malengo zinahitajika
Ripoti hii inazitaka serikali za nchi mbalimbali kuchukua hatua za haraka kupambana na tatizo hili sugu la ukosefu wa ajira kwa vijana.   Juhudi za pekee pia kutoka kwa vyama vya waajiri na wafanyakazi zinahitajika.  Inasisitiza pia kuwa ni vyema kila nchi ikazingatia maeneo ya sera yaliyopendekezwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwezi Juni 2012.  Hatua zifuatazo zilipendekezwa na taarifa hii:

-         Kulenga kwenye ukuaji wa uchumi unaokuza ajira na kazi zenye staha kupitia sera mbalimbali, sera za soko la ajira, ujasiriamali kwa vijana na haki yao ya kupambana na tatizo la ajira na athari zake, na pia kuhakikisha uwepo wa uwezo kifedha.
-         Hatua za makusudi zichukuliwe zikilenga vijana wenye ulemavu na wasiojiweza hasa kwa nchi zile zenye kiwango kikubwa cha ukosefu wa ajira kwa vijana.  Hatua hizo zijumuishe elimu, mafunzo, kuhimiza mashirika kutoa ajira na kuwasaidia vijana kupata uzoefu katika kazi.
-         Kuandaa mikakati na mipango ya kuwapatia vijana ajira na kipato has katika nchi zinazoendelea ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo, kuwapatia ujuzi katika kazi na mbinu za ujasiriamali na uendeshaji wa biashara.

Kwa maelezo zaidi wasiliana nasi:  ILO Office Dar es Salaam, P. O. Box 9212, Tel: 2196700, Fax: 2126627, Email: daressalaam@ilo.org  au ILO Department of Communication, Geneva, at: +4122/799-7912, communication@ilo.org,
Labels:

Post a Comment

Author Name

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.